AVEVA AMKANA DONALD NGOMA KWEUPEE... asema uvumi wa kufanya mazungumzo nae ni mpya kabisa masikioni mwake

KLABU ya Simba imesema haijafanya mazungumzo na straika wa kimataifa wa Yanga raia wa Zimbabwe, Donald Ngoma.

Rais wa Simba, Evans Aveva amekaririwa akisema kwamba jambo hilo ni geni kwake na kama limefanyika basi itakuwa limefanywa na watu wengine.

Kumekuwa na habari zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii kwamba Simba imefanya mazungumzo na Ngoma lakini uongozi wa Simba umekanusha jambo hilo.

Hata hivyo, chanzo kimoja kimesema kuwa Ngoma amefanya mazungumzo na Simba kwa nia ya kujiunga na timu hiyo msimu ujao baada ya mkataba wake kumalizika ndani ya Yanga.

“Simba imefanya mazungumzo na Ngoma na kuonekana kwamba wamekubaliana baadhi ya mambo ambapo kama hali ikienda vizuri basi msimu ujao atavaa jezi za Simba baada ya mkataba wake kumalizika ndani ya Yanga,” kilisema chanzo hicho.

Kama usajili huo utakamilika, basi Ngoma aliyetua nchini miaka miwili iliyopita akitokea FC Platnum ya nyumbani kwao, atajiunga bure na Simba, huku timu yake ya sasa, yanga ikikosa fedha za usajili wake kutokana na mkataba wake kumalizika.

Lakini Aveva amesema kwamba yeye binafsi taarifa hizo hazijamfikia na kama zipo basi labda itakuwa Kamati za chini yake ndizo zinafahamu kila kitu juu ya jambo hilo.


Kamati ya Usajili ya Simba iko chini ya mwenyekiti wake, Zakaria hans Poppe pamoja na wajumbe wengine “makini” na wanasemekana kuweza kufanya lolote kwa wakati wowote.

Labels: